‘A’ HADI ‘Z’ ZA KUZINGATIA KWA MCHUMBA ANAYEPASWA KUWA MWENZI WA MAISHA



     Kumekuwapo na changamoto nyingi sana za ndoa, na hizo changamoto zimesababishwa na kufanya makosa kwa wanandoa hapo awali katika suala nzima la uchaguzi wa wenzi au wachumba wao katika hatua za uchumba kabla ya ndoa kuja. Changamoto mojawapo katika ndoa imesababishwa na mitazamo tofauti na utashi binafsi wa watu katika kuingia kwenye ndoa.
     Kutokufahamu umuhimu wa ndoa kwa Wakristo baadhi kumepelekea kuvunjika kwa ndoa baadhi, maana wanandoa hao wameoana kwa kuangalia vitu, kazi, mali, sura, kipaji, mvuto, umaarufu au cho chote kutoka kwa mchumba kama kigezo cha kumvuta na kuiingia katika mahusiano ya uchumba ili kuifikia hatua na adhima ya ndoa.
     Ndoa (kama tasisi) ni takatifu, na Mungu aliiasisi ndoa kwa makusudi matakatifu. Ndoa ya kwanza iliasisiwa na Mungu mwenyewe katika bustani ya Edeni kati ya Adamu na Hawa (mume mmoja na mke mmoja). Hivyo basi, mchakato mzima wa kumpata mwenzi wa maisha kunahitaji kumshirikisha Mungu ili akupatie mwenzi mwema wa maisha wa kufanana nawe. Vijana wa kike na wa kiume wanaotegemea kuingia katika ndoa, wanatakiwa wajue kuwa, kunahitajika uangalifu mkubwa sana ili kumpata mchumba na mwenzi sahihi wa ndoa.
     Hivyo; ni vyema kutambua ni kipi cha kuzingatia ili kumpata mchumba anayefaa kuwa mke au mume mwema. Mithali 2:11 inatuambia kuwa: “Busara itakulinda; Ufahamu utakuhifadhi”. Kwa hiyo, sehemu yote ya sura hii itatoa elimu, busara ufahamu ambao vijana wa kike na wa kiume utawahifadhi kwa kufuata hatua zitakazokuwa za msingi katika kujipatia mchumba anayestahili kwa ajili ya ndoa yenye furaha daima:

‘A’Azima ya Kuingia Kwenye Ndoa Itambuliwe
     Azima na nia ya kuingia kwenye ndoa yampasa mtu aitambue. Jambo la kuwa katika ndoa halikwepeki, muda ukifika wakufanya hivyo yampasa mtu kuazimia kwa dhati kabisa. Biblia inasema kwenye kitabu cha Mhubiri 3:1 “Kwa kila jambo kuna majira yake na wakati kwa kila kusudi chini ya mbingu”. Kunuia kwa mtu na kuwa tayari kutamwandaa kisaikolojia pamoja na kujipanga kwa ajili ya azima hiyo. Kwa namna nyingine, kuingia kwenye ndoa sio suala la kuigiza wala kujaribu, bali kunahitaji azima ya kuingia kwenye ndoa moja kwa moja.

‘B’Bidii ya Kazi
     Mchumba anayefaa ni yule mwenye bidii katika kazi na siyo alichonacho, mali alizonazo, kazi aliyonayo nk. Mtu mwenye bidii katika kutafuta anauhakika wa kufanikiwa, hivyo mchumba huangaliwa katika kufanya kazi kwa bidii na mipango thabiti kwa ajili ya kuyatafuta mafanikio kwa njia halali. Mithali 10:4 na Mithali 12:27; mafungu haya yamesadiki juu ya bidii katika kazi. Kulingana na mfumo wetu wa elimu (miaka 16 na zaidi hutumika kwa ajili ya elimu toka chekechea hadi chuo kikuu). Kumpata kijana aliyefanikiwa kuwa na funguo tatu yaani nyumba, ofisi na gari ni nadra sana. Mara nyi watu hupata funguo tatu uzeeni na umri wa kuoa unakuwa umepita. Hivyo, angalia mchumba aliye na bidii katika kazi, ili muyatafute maendeleo katika ndoa kwa pamoja.

     Hivyo kwa wale wanaotafuta wenzi wenye funguo tatu hasa kwa kijana, yampasa amtafute mtu mzee, mtu aliyefiwa na mwenzi wake au kwa binti aingie katika ndoa ya mitara. Mchumba mvivu na tepetevu na asiyejibidisha hafai kuwa mke au mume kwani dunia ya sasa inahitaji kusaidiana katika kutafuta ili kuyafikia malengo mapema. Huu ni ushauri wangu mwenyewe, maana uzoefu unaonesha madhara yake. Mfano baba ambaye ni mtafutaji pindi anapofariki au kupata ulemavu wa kudumu au ugonjwa wa kudumu, familia huyumba na kusambaratika. Hili jambo lipo hata kwa upande wa wanaume, maana wapo wasiotafuta wala kujibidisha katika kutafuta hivyo kutegemea mahitaji yaliyo mengi kutoka kwa wake zao (ambapo sio salama pia).

‘C’Chunguza Tabia
     Kipengele hiki ni nyeti sana maana ndipo kiini cha mchumba anayefaa kuwa mke au mume. Kipengele hiki kinabeba muktadha mzima wa mchumba mwema atokaye kwa Mungu. kupitia tabia ndipo unaweza kupata mke mwema.  Wasifu wa nje wa mtu kuutambua ni rahisi sana kuliko wasifu wa ndani wa mtu; vivyohivyo tabia za ndani na tabia za nje kwa mchumba. Ukikosea kuchunguza tabia ya mchumba katika kipindi cha urafiki, ni vigumu kuzibaini tabia katika uchumba maana atazificha ili kulifikia lengo la kuolewa au kuoa.

     Tabia ni sawa na ngozi, kuibadirisha ni vigumu sana (Yeremia 13:23). Usijipe moyo kwa kusema na kufikiri “ngoja anioe au nimuoe kisha nitambadirisha tabia yake”. Japo pia mwenye uwezo wa kumbadirisha mtu tabia ni Mungu, hivyo itahitaji maombi mengi na ya dhati kwa kumuombea mchumba au mume au mke. Mafungu yaliyo katika Mithali 7:10-12, Mithali 11:16 na Mithali 12:4 yanaeleza juu ya tabia bainishi zinazofaa na zisizofaa kwa mtu anayemwabudu na kumcha Mungu wa mbinguni. Kuna aina kuu mbili za tabia na mfano wake:

     1. Tabia zinazojipambanua kwa nje: Tabia za nje zinajipambanua katika matumizi ya ulimi wakati wa kuongea, mitindo au aina za mavazi anazo pendelea kuvaa (Mwanzo 3:7, Kumb 22:5, 1pet 3:1-6), kujipamba kwake kwa sura au mwili na manukato (Hosea 2:13, Wimbo 1:3, Ezekiel 23:40), vyakula na vinywaji apendeleavyo (Mithali 23:20-21). Tabia zote za nje kuzibaini hazihitaji muda mrefu sana, mfano, si vigumu kumbaini mtu mchafu au msafi.

     2. Tabia zinazojipambanua kwa ndani: Tabia hizi hazionekani kwa urahisi maana ni za ndani mno; mfano wa hizo ni wivu, upole, uchoyo, kutojali, dharau, mtazamo kwa kutaja baadhi. Tabia za ndani huchunguzwa kwa muda mrefu sambamba na matendo ya huyo mtu. Warumi 3:12 imezungumzia tabia njema zinatakiwa kuwa hata za moyoni. Ugunduzi wa tabia hizi juu ya mtu, kunahitaji kiwango na ujuzi mzuri wa saikoloji. Kubadilika kwa tabia hizi za ndani kunahitaji uwezo wa Roho Mtakatifu na utayari wa mtu baada ya kugundua udhaifu na mapungufu yake.
‘D’Dini au Dhehebu
     Dini au dhehebu katika mahusiano ni kipengele cha kuzingatia na kutilia maanani zaidi. Inapendekezwa kuwa, wale wanaotarajia kuwa wenzi ni vyema ukawepo ufanano wa dini au dhehebu. Kila dini na dhehebu kuna mafundisho yake (doctrines) ambayo yanapishana kutoka dhehebu au dini moja kwenda dhehebu au dini nyingine.  1Wakorintho 1:10 na 1Wakorintho 1:12 aya hizi zinatoa umuhimu na faida za wanandoa kuwa wenye dini au dhehebu moja, maana hawatapishana katika misingi ya mafundisho bila kuwagawanya watoto katika imani za mafundisho. Ukitaka familia iwe chini ya kiwango katika mambo ya kiroho, jaribu kuchanganya dini mbili tofauti miongoni mwa wanandoa katika ndoa.

‘E’Elimu
     Kuna elimu ya kweli ambayo inahusu uelewa na maarifa juu ya Mungu wa kweli wa mbinguni na elimu ya kidunia ambayo tunaipata shuleni kupitia mitaala ya masomo mbalimbali. Nitazungumzia juu ya elimu ya kidunia ambayo inaweza ikaleta utofauti kwa wachumba watakapo kuwa katika maisha ya ndoa. Inashauriwa kuwa wachumba wanaotarajia kuoana wasipishane sana viwango vya elimu au walingane viwango vya elimu ili kuleta uwiano katika mitazamo, uelewa na tafakari.

     Sanjali na viwango vya elimu kuwiana au kutotofautiana, kigezo cha elimu lazima kipewe nafasi ili kila mmoja kati ya wachumba kuridhia wao kwa wao, endapo mmoja hajui kusoma wala kuandika au hajaenda vidato katika elimu. Suala la elimu pia laweza kutatuliwa kwa wenzi kukubaliana katika kuendelezana katika masuala ya elimu. Mafungu yafuatayo yanaelezea juu ya elimu ya kweli na elimu dunia: Mithali 4:13, Waefeso 5:22 na Esta 1:22.

‘F’Familia Atokayo (Historia yake)
     Suala la ufahamu wa historia na familia anayotoka mchumba ni vyema kuifahamu bayana na kujiridhisha kwayo. Kuifahamu familia anayotoka mchumba ni jambo jema sana, kwani itasaidia kujua endapo kuna magonjwa ya kurithi, malezi mabaya na tabia mbaya za wazazi au walezi wa mchumba ama sivyo. Mara nyingi tabia ya wazazi au mzazi (walezi au mlezi) hubainisha tabia ya mchumba, hususani binti kama anavyoelezwa katika Ezekieli 16:44.

     Mafungu mengine yanayoelezea juu ya umuhimu wa kuijua historia ya familia anayotoka mchumba ni Hosea 2:4-5 na 2Samweli 13:8-12. Yapo matendo yaliyofanywa na wazazi na kupelekea matokeo yake kuendelea kuandama vizazi vinavyofuata (Kutoka 20:5) hivyo ni bora kujiridhisha kabla ya kuoa au kuolewa.

‘G’Gharama ya Mahali kwa Mchumba
     Kila jambo halikosi kuwa na gharama aidha muda au pesa. Zipo gharama kwa mchumba, hivyo ni vyema (kijana wa kiume) akazitambua ili kujua endapo atazimudu ama sivyo. Ipo gharama kubwa ambayo huwa inawakabili vijana wa kiume ni lazima aipitie ili kuifikia hatua ya kumuoa mchumba aliyempata.      

     Gharama hiyo huhusisha mahali pamoja na viambata vya zawadi (Mwanzo 24:48-53). Suala la mahali linatofautiana tamaduni na tamaduni, sehemu na sehemu, imani moja kwenda imani nyingine.

     Nionavyo mimi: ifike wakati Wakristo tuachanane na suala la mahali ili tuepukane na tamaduni katika mchakato wa ndoa. Mahali sio kitu kizuli maana taratibu zake zimejaa upagani mwingi. Suala la mahali kuwa ghali, limekuwa kikwazo kikubwa katika jamii ya Wikristo hususani kwa kusababisha vijana wasioane; hivyo, vijana kuoana bila kufuata taratibu za Kibiblia,  mabinti kutoolewa na mwisho wa siku kuzaa watoto nje ya ndoa aidha wakiwa bado nyumbani kwa wazazi wao.

     Aidha, kwa upande wa kijana wa kiume lazima aangalie gharama za maisha ya binti kulingana na familia anayotoka ili kujua kama ataweza kumhudumia katika ndoa. Zipo familia ambazo zipo vizuri kimaisha (kiuchumi), hivyo kunamaisha ya hali ya juu ambayo mtoto wa kike amekuwa akiyaishi na kila alichohitaji alikipata. Kijana anaetarajia kuoa binti atokaye katika familia tajiri lazima ajiandae kumhudumia kama alivyokuwa akiishi nyumbani kwao. Kwa mtazamo wangu pesa sio tiba ya kuleta upendo bali upendo wa dhati unatoka moyoni mwa mtu husika. Soma  Mithali15:16-17. 

‘H’Hiari ya Mchumba Kuishi Naye
     Upendo wa kweli hauhitaji shuruti wala kulazimisha, bali upendo huandamana na hiari juu kuridhia toka moyoni. Hivyo, mchumba ni vyema akakubali yeye mwenyewe ili kuingia ndani ya ndoa. Uhuru katika kukubari hakuleti majuto hapo baadae ndani ya ndoa, maana mtu ameamua mwenyewe. Sio salama sana kutumia ushawishi wa kipesa, mali au misaada yo yote ili kutengeneza mazingira ya mchumba kukubali, kwa sababu vitu au pesa vyaweza kuwa mvuto bandia badala ya upendo wa kweli kutoka moyoni.

     Rushwa yenye ushawishi katika uchumba si jambo jema, maana hapo baadae kwa wenzi, kunaweza kukatokea upungufu au ukosefu wa upendo wa dhati ndani ya ndoa. Kunajambo zuri la kujifunza katika Mwanzo 24:54 ambapo Rebeka alihiali yeye mwenye kwenda kuungana na mume wake baada ya kutolewa zawadi na mahali.


‘I’Imani
     Kipengele hiki ni sawa na kile kipengele cha dini au dhebu, lakini kinautofauti kidogo. Suala la imani nalo ni jambo nyeti sana sawa sawa na kile kipengele cha “D” juu ya umuhimu wa wachumba kufanana kwa dhehebu au dini kabla ya kuoana. Yapendeza wachumba wanaotaka kuoana wawe wa imani moja, maana kutofautiana imani huzaa migogoro katika ndoa.

     Zipo imani ambazo huruhusu kula vyakula vyote, kuoa na kuacha (kutalakiana), kunywa pombe, kuoa wake wengi na kuvuta sigara, hivyo mwingine akiwa na masharti katika hivyo vipengele, kutaleta migogoro mikubwa ndani ya ndoa. Sambamba na hayo, hata taratibu za ibada kupisha kati ya imani moja na nyingine kwa wenza husababisha makwazano miongo mwa wanandoa.
     Suala lingine la msingi katika imani ni juu ya kiwango cha kiroho cha mchumba. Inapotokea wachumba ni wa imani moja, suala la kiwango cha kiroho (imani) kwa mchumba lafaa kuzingatiwa pia ili hapo baadaye wachumba hao watakapooana waweze kuwa na familia yenye kiwango kizuri cha kiroho pamoja na malezi mazuri ya kiroho kwa watoto wao.
     Sio salama pia kutumia silaha ya kumtangazia mtu (mchumba) kuwa nitaolewa au nitakuoa wewe endapo utabadiri imani yako na kuja kwenye imani yangu; kwa sababu mchumba aweza kukubali kubadiri imani yake ili aolewe au kuoa kwa sababu ya kukidhi hitaji lake na siyo kwa kuikiri imani.
     Kitabu cha 1 Wafalme 11:4 kinasema hivi: “Maana ikawa, Sulemani alipokuwa mzee, wake zake wakamgeuza moyo wake, afuate miungu mingine, wala moyo wake haukuwa mkamilifu kwa BWANA Mungu wake, kama moyo wa Daudi baba yake.” Ni vyema wachumba wanaotarajia kuoana wawaze pamoja, wanuie pamoja, watende pamoja, waamini pamoja katika imani ili kuondoa mpasuko hapo badae wawapo kwenye ndoa yao.
‘J’Julisha Wazazi
     Uchumba wa “Yusufu na Mariam” ulitambulika nyumbani kwao na jamii inayowazunguka. Wakati mwingine hata urafiki utambulike kwa wazazi ili wazazi nao wapime uaminifu wa rafiki huyo kama ilivyotokea kwa Musa (Kutoka 2:16-21). Wachumba wanaotarajia kuoana ni vyema wakazijulisha pande zote mbili za wazazi wao ili kuweka uwazi na kulinda uchumba wao ili kuepuka usaliti kama ambavyo wangekuwa wawili kwa uchumba wa siri.

     Huwa ni moja ya heshima kubwa sana kwa wazazi kujulishwa juu ya uchumba wa binti au kijana wao endapo amefikisha umri wa kufanya hivyo ili nao wapate ya kushauri au kutoa baraka zao kwa ajili ya hatua nyingine kuelekea katika ndoa.



‘K’Kasoro Alizonazo Mchumba Zibaini Mapema
     Kubaini kasoro alizonazo mchumba ni vyema na ni vizuri ili kujipima kama zitaweza kuvumilika au kubadirika kama ni za kufanyiwa mabadiriko haraka kabla ya kuamua kuingia kwenye ndoa. Biblia inamzungumzia “Lea” kasoro yake ya kuwa na makengeza lakini Yakobo alimkubali kwa kasoro yake hiyo (Mwanzo 29:17). Lea huyo huyo mwenye kasoro na asiyependwa alibarikiwa kupata mtoto mapema kuliko “Raheli”. (Mwanzo 29:31).

     Hakuna mtu ambaye hakosi kasoro, labda awe malaika. Lakini, ni vyema kufahamu kuwa; kasoro ambazo sio za kimaumbile bali ni za kitabia huachwa na si za kuvumiliwa. Ukizibaini kasoro zako pia yakupasa kuziacha.

‘L’Linganisha Umri wenu
     Nionavyo mimi: jambo la msingi kutambua katika umri; wanawake hukomaa kiakili mapema, kuliko wanaume; lakini pia wanawake hukua kiumbo haraka, lakini hawazeheki mapema, bali wanaume hawakui haraka ila huzeeka mapema. Hivyo basi ni vyema mwanamke awe chini kidogo ya umri wa mwanamume kutokana na kukua kwao haraka.

     Ulinganifu wa kiumri ni mzuri ili kubaini umri sahihi wa kuzaa pamoja na kuweza kusimamia majukumu ya kifamilia. Kiafya inashauriwa kuwa, mwanamke asiendelee kuzaa afikishapo umri kati ya miaka 34 hadi 36, hivyo ili mwanamke aweze kuzaa watoto watatu wenye kutofautiana miaka mitatu; akichelewa sana mwanamke aanze kuzaa akiwa na umri wa miaka 25 hadi 26 ili ukijumlisha miaka tisa ya tofauti ya watoto watatu, hivyo atakoma kuzaa akiwa au kabla ya miaka 36. Jambo la kusisitiza ni kuwa si wote wanaoweza kutendewa miujiza kama Sara alivyo zaa katika umri wa uzee (Mwanzo 17:17).
      Sio vizuri pia kwa mwanamume kuchelewa kuoa, maana haipendezi kulea watoto katika umri wa uzee, hivyo angalau mtu akichelewa sana miaka 32 awe ameoa. Sanjali na hayo, kwa mtazamo wangu: umri wa miaka 18 hadi 25 kwa wanawake huwa ni umri wa mabadiriko makubwa ya kimaumbile, na wengi wao hunenepa kutoka umbo la awali kwa sababu ya mabadiliko ya kihomoni na maumbile. Umri wa miaka 25 na kuendele ndio umri sahihi wa kutambua umbo la mwanamke maana atakuwa amepitia hatua zote za mabadiriko ya kimakuzi.

‘M’Miliki Alizonazo Mchumba Zitambulike
     Vijana wengi huwa hawana mali kwani huwa katika hatua za utafutaji wa mali. Endapo kuna mali au miliki aidha za kurithi au kupewa na ndugu au jamaa;  kunatakiwa kuwepo ukweli na uwazi kwa wachumba juu ya mali na miliki walizonazo kwa kila mmoja kabla ya kuoana. 

     Kukosekana kwa uwazi juu ya miliki au mali alizonazo mchumba kwa weza sababisha kutoaminiana endapo siku moja miongoni mwao katika ndoa atabaini kuwa hakuwekwa wazi. Kumficha mchumba juu ya miliki na mali hupelekea kupotea endapo mmoja atafariki ghafla wakati wawapo katika ndoa. Uwazi wa miliki utawaweka huru wachumba wote wanaotaka kuoana hapo baadae ili kurahisisha mipango ya maendeleo yao mapema.
     Wakati mwingine mali alizonazo mchumba hujulikana bila hata kumuuliza mhusika, kama ilivyokatika kisa cha kitabu cha Ruthu, ambapo Ruthu alitambua mali za Boazi kwa kumuona katika usimamizi wa hiyo miliki yake (Ruthu2:3-4). Jua kuwa: Boazi alikuwa mzee katika umri, hivyo mali zake alikuwa amezitafuta tangu enzi za ujana wake, hivyo ni tofauti na vijana wengi ambao huwa hawana mali, kwani huwa katika mchakato wa kutafuta mali.

‘N’Ndoto za Mchumba Katika Maisha yake
     Kila mwanadamu aliye na akili timamu na mwenye uwezo wa kufikiria japo hata kidogo huwa hakosi kuwa na ndoto za maisha anazotarajia kuzitimiza katika kipindi cha muda fulani ndani ya maisha yake. Ni vyema ndoto za wachumba zibainike kwa kila mmoja, ili waweze kuona namna na jinsi yakuweza kuzitimiza aidha ndani ya ndoa au kabla ya ndoa.
     Aidha, mmoja wao kati ya wachumba anaweza akawa na mpango wa kufikia kiwango fulani cha elimu, mfano shahada ya kwanza katika taaluma fulani ndipo aoelewe, hivyo ni vyema mwingine kuvuta subira ili lengo la mchumba wake litimie katika ndoto ya maisha yake. Endapo itakuwa ni vigumu kusubiri, basi huyo asiyeweza kusubiria amuache mchumba wake na awe huru kutafuta mwingine aliyetayari kuingia katika ndoa bila kupoteza muda mwingi.

‘O’Onesha Hali Halisi ya Maisha Yako
     Kitendo cha kuonesha hali halisi ya maisha hata kabla ya uchumba na ndani ya uchumba ni jambo jema na salama sana. Inawapasa wachumba kuepuka maisha ya kuigiza tofauti na jinsi walivyo, maana ni mojawapo ya udanganyifu na huleta migogoro hapo baadaye katika ndoa. Unakuta kijana anaazima gari, nguo ili aonekane ni wa maisha ya juu sana na kushawishi wale wa karibu yake waone kuwa ni mtu wa maisha mazuri.
     Ukiazima gari, eleza kuwa umeazima na kuazima nguo kumepitwa na wakati na hakufai kabisa. Kitendo cha kuigiza hali ya maisha yasiyo “Ruthu” alikishinda, zaidi alionesha hali ya maisha yake jinsi yalivyo toka moyoni hadi nje ya maisha aliyokuwa akiyaishi; angalia Ruthu 1:16-17, Ruthu 3:10. “Esta” naye katika nchi ya ugenini pia naye alifanya vivyo hivyo hadi kupata fursa ya kuolewa na mfalme, maana mabinti wengi walienda kwa kujipamba, kuvaa vito na mavazi ya thamani sana wakati siyo hali ya maisha yao; Esta yeye alienda jinsi alivyo (Esta 2: 15-17).
     Tabia ni uchaguzi mtu anaweza akaibadirisha endapo akinuia kufanya hivyo kwa dhati. Vijana wa kiume na wakike yawapasa kuishi katika kweli na ukweli mtupu ili ukweli uwaweke huru. Katika uchumba wamo matapeli wengi sana, ndiyo maana wengi huumizwa sana punde ibainikapo kuwa mchumba huyo sivyo alivyokuwa akimdhania na kujitumainisha kwake.


‘P’Pima Uaminifu wa Mchumba
     Uaminifu hauwezi ukaondolewa na mazingira, sababu fulani wala changamoto inayomkabiri mchumba. Kuanza uhusiano (kuoa na kuolewa) na mtu ambaye hujajihakikishia upendo na uaminifu wake juu yako ni kujipalia moto hapo badae; maana wapo ambao huanzisha mahusiano na mtu fulani kwa kutimiza haja zao za matamanio au kuchuma kitu fulani kwa huyo mtu.
     Kwa wale wanaoelekea katika safari ya maisha ya ndoa na ambao bado wanatafuta; kipindi salama cha kumchuguza tabia mtu, ni kipindi cha urafiki na kidogo kipindi cha uchumba. Kijana wa kiume akimtamkia binti kuwa anataka kumuoa (yaani awe mchumba), matarajio ni kuwa, huyo binti ataficha tabia ake mbaya alizonazo ili aolewe. Vivyo hivyo kwa binti anapomkubalia kijana wa kiume kuingia naye uchumba, ategemee pia kijana huyo atazificha tabia zake mbaya ili aweze kufanikisha kumuoa. Wote hao; kijana wa kie na wa kiume wakifika kwenye ndoa hujibainisha tabia zao zote mbaya, ambapo kuzirekebisha kunahitajika hekima ya kimbingu ya wanandoa na Mungu aingilie kati.
‘R’Ruhusa ya Wazazi
     Ruhusa toka kwa wazazi huwa ni jambo la msingi sana kwa wachumba ili kuweza kuoana. Mbaraka wa wazazi ni bora na mhimu kwa wachumba katika safari ya kuoana na kuanzisha familia. Tena ni vyema pande zote za wazazi zikaridhia ili wachumba kuendelea na mchakato wa kufanikisha ndoa. Kuridhia kwa wazazi hutengeneza upendo kila upande wa wazazi wa wanandoa katika familia (soma Mwanzo 29:21-23).
     Japo kunawakati pia wazazi hupinga kulingana na mila, wakati mwingine utashi wao au imani, hivyo mtii baba na mama katika misingi ya Kibiblia na sio misingi iliyo nje na neno la Mungu. Hekima ya wachumba katika kushauri itumike pale inapoonekana kuwa wazazi hawako sahihi kwa yale wanayolazimisha kulingana na neno la Mungu linavyo elekeza, na pia mazuri yaliyo mema ya wazazi wachumba wayafuate na kuyatii. 
     Samsoni mnadhiri wa Mungu alipingwa na wazazi wake kwa jambo jema kabisa; yeye mwenyewe alikengeuka kwa utashi wake mwenyewe. Ukisoma “Waamuzi 14:1-4” inaonesha kuwa wazazi wake Samsoni walimpinga kwa ombi lake baya. Maamuzi yake Samsoni yalikuwa kinyume na imani kama mnadhiri wa Mungu hivyo ilimgharimu mateso na hadi kifo akiwa mateka katika himaya ya Wafilisti waabudu miungu.

‘S’Sura na Umbo la Mchumba
     Ni vyema kuchagua mchumba utakayempenda daima wakati wote wa maisha ya ndoa kwa kuzingatia uzuri wa tabia kwanza na uzuri wa umbo. Kila mtu ni mzuri kwa asili yake, kulingana na muonekano wa nje au tabia za ndani. Biblia inazungumzia sana uzuri wa asili na uzuri wa tabia na sio uzuri wa kununua au mapambo ya gharama na vito vya thamani. Katika lugha yetu ya Kiswahili ni vyema ukatofautisha uzuri na urembo au ulimbwende.

     Uzuri ni wa asili, urembo au ulimbwende ni mapambo na muonekano wa mavazi katika mwili. Japo uzuri na urembo huenda pamoja na huwezi ukautofautisha kwa uharaka; maana wapo wazuri kwa sababu ya mapambo na mavazi, na wapo wabaya kwa sababu ya kukosa mapambo na mavazi nadhifu.
     Soma mafungu yafuatayo: Esta 1:19 inazungumzia ukarimu, Mwanzo 26:7 inazungumzia uzuri wa Rebeka, Wimbo 2:14 inazungumzia uzuri wa umbo na sauti, Wimbo1:15 inahusu uzuri wa mwanmke, Wimbo 5:10 inasifu rangi na umashuhuri na Esta 2:7 inasadiki uzuri wa sura na tabia njema.
‘T’Tamaduni Zenu Zisitofautiane Sana
     Suala la tamaduni huleta changamoto na tofauti nyingi sana na hupelekea kutokea kwa migogoro katika ndoa; hivyo ni vyema pia kwa wachumba kabla hawajaoana lazima waliangalie hili ili lisije likawa changamoto aidha wao kwa wao au kutoka kwa ndugu zao (angalia Mwanzo 28:2 na Waamzi 14:1-3). Kwenye biblia hasa agano la kale, suala la utamaduni limejitokeza katika mgongo wa imani kama inavyotanabaishwa katika mafungu tajwa hapo juu. Agano jipya halitilii sana mkazo wa tamaduni bali imani.
     Endapo Imani ni moja, suala la utamaduni halipo. Hakuna tamaduni iliyobora kuliko nyingine, isipokuwa ni mitindo tu ya maisha ndiyo huleta tofauti ya tamaduni moja na nyingine. Watu wa imani moja si sawa kulishupalia suala la utamaduni maana huleta utengano na ubaguzi. Kwa sasa kutokana na kuingiliana, kuoleana na msingi wa utamaduni wetu upo juu ya tabia ya Yesu Kristo; tamaduni zetu hazina nafasi tena, bali hoja ya msingi ni imani hazitakiwi kutofautiana kama ilivyonenwa katika Mwanzo 24:3-4.

‘U’Ukarimu na Uvumilivu wa Mchumba
     Kipengele hiki kitamhusu sana mwanamke na kiasi mwanamume, maana mwanamke ndio muhimili mkuu wa familia japo baba ndiye kichwa cha familia. Mwangalie mchumba wako Je, anaweza kuvumilia katika shida bila kusaliti anapoishiwa? Mwanamke katika ndoa na familia yake, awe na moyo wa ukalimu, huruma, kutoa na kusaidia wengine walio wahitaji (soma Mithali 31:20). Baadhi ya wanawake wana roho mbaya na hawana hata tone moja la ukalimu na moyo wa kusaidia wengine; wakati mwingine huwabagua wale wasio wa upande wa familia yake (suala hili lipo hata kwa wanaume pia).
     Mwanamke anayemcha Mungu ni sehemu ya kimbilio na msaada kwa jamii na wanafamilia wanaomzunguka. Moyo wa kutoa, kusaidia wahitaji na masikini pamoja na kuwakalimu wageni ndizo funguo za baraka ya familia. Roho mbaya na ukali hukimbiza wageni katika familia, na kupelekea kufunga milango yote ya baraka kutoka kwa Baba wa Mianga. Mwanamke mwanandoa mtarajiwa lazima ajenge tabia ya kuvaa viatu vya matatizo ya wengine, ahurumie na kukumbuka kuwaombea walio katika shida na changamoto.
     Mwanamke ambae ni mke mtarajiwa yampasa kuwa mwangalifu ili kujipatia mume mwenye tabia njema. Katika 1Samweli 25:1-42, mtumishi wa Mungu Daudi alipanga kumwangamiza Nabali kwa sababu ya kukosa hekima ya maneno na fadhira juu ya yale Daudi aliyomtendea katika kumlindia mifugo yake, lakini   Abigaeli mkewe Nabali alijishusha kwa Daudi; kwa kutumia hekima na maneno mazuri alifanikisha kumuepushia mumewe na upanga wa Daudi.

‘V’Vumilia Mapungufu Aliyonayo Mchumba Ikiwezekana
     Kama tulivyoona kwenye kipengele cha kubaini kasoro za mchumba, kuwa hakuna mwanadamu aliyekamilika asilimia mia. Ukimpata asiyekuwa na kasoro au hana mapungufu, tegemea malaika pekee na ambapo hapa duniani hayupo. Yapo mapungufu mengi ambayo yanaweza kujipambanua kutokana na silika ya dhambi kwa mwanadamu. Mapungufu hayo yanaweza kuwa yaliyo katika nyanja kuu mbili, yaani mapungufu yatokanayo na wasifu wa nje (mapungufu ya kimaumbile) na mapungu yatokanayo na wasifu wa ndani (matendo ya kiroho zaidi, mfano uchoyo, hasira, kiburi n.k).

     Suala la kumvumilia mchumba kutokana na mapungufu yake ni kanuni ya kimbingu kama jinsi Mungu anavyotuvumilia kwa hali ya juu. Kuvumilia pekee hakutoshi, bali muombee, mwelekeze kwa upole na kumfundisha kwa moyo wa upendo. Kwa mtazamo wangu; tabia ni uchaguzi tofauti na kalama ambapo Mungu humpatia mtu.

     Mungu anasehemu kubwa sana ya kutubadirisha kuliko tunavyoweza kufikiri na kufanya kwa uwezo wetu. Tukimshirikisha Yeye aweza kutubadirisha na kuwa nuru au chumvi ya ulimwengu. Mungu alimbadirisha Petro, Paulo; hivyo tukimwomba kwa nia ya dhati atatubadirisha au kubadirisha tabia ya mchumba usiyoipenda.

‘W’Wasilianeni Mara kwa Mara
     Kuwasiliana ni mojawapo ya kanuni inayoweza kufanikisha kudumu kwa uchumba endapo wawili miongoni mwa wachumba wako mbali kimazingira. Kuwasiliana mara kwa mara kunasaidia kujenga uhusiano na kutambuana mapungufu au matatizo, hata kukuza upendo wa wachumba. Uchumba waweza vunjika kwa sababu ya kukosekana kwa mawasiliano ya karibu na ya mara kwa mara.

     Bila mawasiliano kutokana na umbali, mchumba anaweza kumsahau yule wa mbali endapo atajitokeza anayeonesha kujari kwa ukaribu na kumjulia hali au kuzungumza naye mara kwa mara. Zipo njia nyingi za kuwasiliana kwa ulimwengu wa sasa; kuwasiliana kwa weza kuwa katika kuombeana, kuwasiliana kwa kutumia simu, barua kwa njia ya posta, barua pepe na mitandao ya kijamii.

     Mfumo wa maisha wa sasa haulingani na mfumo wa maisha ya babu zetu wa zamani, vivyo hivyo uvumilivu na uaminifu bila kuvunja uchumba kwa hivi sasa hauwezekani kwa sababu ya kukosa mawasiliano kwa dunia ya sasa ya sayansi na teknolojia. Kuwasiliana kunakumbusha kutunza ahadi ya wachumba ili kulifikia lengo lao la kuoana. Kuwasiliana pia kunaonesha upendo katika kumjali mchumba ili aonekane kuwa ni wa thamani, pamoja na kutiana moyo ili kuvishinda vishawishi.
‘Y’Yakinisha Pendo la Mchumba
     Kwa mujibu wa 1Wakorintho 13:4-13; upendo ni uwazi, upendo ni uvumilivu, upendo hauchoshi, upendo huwafanya wapendao kubebeana matatizo na shida, upendo ni furaha, hivyo upendo haujifichi. Ni vyema mchumba akaangalia nakuchunguza kweli ya upendo wa mchumba wake. Mchumba aliye na upendo wa kweli, atamuweka mchumba wake kama muhuri moyoni mwake.
    
     Katika kitabu cha Waamuzi sura ya 16, upendo wa “Delila” kwa Samsoni” haukuyakinisha upendo wa kweli ukiachana na suala la uzinzi na uasherati kabla ya ndoa. Upendo wa Adamu kwa Hawa ni upendo wa kuigwa kwa wachumba (ila si kwa kumuasi Mungu kama alivyofanya Adamu). Kisa hiki cha Hawa na Adamu wengi hukichukulia juu juu; unajua haikuwa rahisi sana kwa Adamu kufanya kosa la kula tunda alipoletewa na Hawa. Adamu alikubali kula tunda kwa sababu ya upendo kwa mke wake, kuwa asiangamie peke yake (Mwanzo 3:6).

     Tufanye nini maana Yesu ameturejeshea kile tulichokipoteza kutoka kwa wazazi wetu kwenye bustani ya Edeni maana ni upendo mwingine waajabu wa agape, Yesu kukiacha kiti chake cha enzi ili atufie siye tusiostahili. Hivyo, upendo ulilipwa kwa upendo wa juu zaidi. Naamini kuwa; kuoa au kuolewa na mtu usiyempenda kwa dhati toka moyoni hupelekea migogoro katika ndoa na kuingia katika dhambi ya kuchukiana na kuishi kwa kuvumiliana.

‘Z’Zuia Kufanya Ngono Kabla ya Ndoa
     Uchumba wa Yusufu na Mariamu ulikuwa katika kanuni ya kujizuia kufanya ngono hadi ndoa itakapofungwa. Mariamu alikuwa bikira safi hakuwa ameguswa na mwanamume, na Yusufu alijua kanuni ya uchumba kuwa kufanya ngono nje ya ndoa ni kujichumia dhambi ya uzinzi (Mathayo 1:18-24 inaleza kisa chote).  Kumekuwepo na ushawishi mkubwa wa utandawazi na makundi rika yanayoharibu maana ya uchumba, kwa kusababisha vijanawengi kufanya ngono kabla ya ndoa, hivyo kushiriki dhambi ya uzinzi.

     Mwonja asali haonji mara moja, akionja huchonga mzinga daima. Samson alionja mara moja na ikabidi ajenge mzinga (Waamuzi 16:1, na Waamzi 14:7). Thamani ya mwanamume au mwanamke hupotea kwa mchumba wake endapo wachumba hao watakutana kimwili kabla ya ndoa. Kuruhusu ngono kabla ya ndoa husababisha uchumba kuvunjika, maana ile shauku ya kuoana hupotea kwa sababu wachumba wameshajuana tayari, hivyo hufanyika mchakato wa kutafuta mchumba mpya.
     Ngono kabla ya ndoa husababisha maambukizi ya magonjwa ya zinaa, mimba za nje ya ndoa, au kuwa na watoto wengi kwa baba au mama tofauti. Nivyema wachumba wakawa waaminifu hadi ndoa ifungwe ili washiriki zawadi yao kwa uhuru.

     Wataalamu wa mahusiano katika misingi ya Kibiblia, hawashauri uchumba uzidi mwaka mmoja kama hakuna kipingamizi kwa wachumba kuoana. Uchumba wa muda mrefu mara nyingi huvunjika, au husababisha wachumba kufanya ngono babla ya ndoa. Jambo hilo husababisha upendo kupungua au kutoweka kwa sababu Shetani anakuwa ameweka himaya yake, na kupelekea uchumba uvunjike.

     Ndoa ni takatifu, ndoa ni kielelezo cha uhusiano wa mwanadamu na Mungu, au Mungu na kanisa, hivyo ndoa iheshimiwe na watu wote. Shetani huharibu utukufu wandoa ili afanikishe kuharibu familia, kanisa na jamii kwa ujumla; hivyo, yawapasa wachumba kuwa waangalifu daima katika hatua zao za uchumba, na haina haja ya kuchelewa kuoana kama hakuna kipingamizi cha kuwachelewesha.






Comments

Popular posts from this blog

MAJINA YA WANAWAKE KATIKA BIBLIA ‘A’ HADI ‘Z’

SOMO: MADHARA YA KUKATAA KUMTII MUNGU

MFANO WA MPANGO KAZI